School of Humanities and Development Studies
Permanent URI for this communityhttp://41.89.103.50:4000/handle/123456789/40
Browse
Item Uchanganuzi Hakiki Wa Mtindo Na Maudhui Katika Nyimbo Za Kisiasa: Mfano Wa Wasanii Kutoka Kaunti Ya Murang’a(Laikipia University, 2014-10) Munyao, Josephine Kanini.Nyimbo kama zilivyo tanzu zingine za fasihi simulizi huhusisha matumizi ya mitindo changamano katika kuwasilisha ujumbe wa kisiasa. Utafiti huu ulidhamiria kufanya uchanganuzi wa mitindo ya nyimbo za kisiasa zilizoimbwa na wasanii watatu kutoka Kaunti ya Murang’a: Joseph Kamaru, Kamande wa Kioi na John De’Mathew. Ulilenga kutambulisha, kuainisha na kuchanganua vipengele vya kimtindo vinavyotumiwa na wanamuziki hao na athari zake kwa wakaazi wa Kaunti ya Murang’a. Pia, dhima inayotekelezwa na nyimbo za kisiasa katika kaunti hii ilichunguzwa. Utafiti umelenga kuonyesha iwapo kuna aina mahususi ya mitindo inayotumiwa na wanamuziki hawa. Aidha, utafiti huu umejikita katika kuweka wazi iwapo nyimbo hizi huathiri maamuzi ya wanajamii wa Kaunti hii. Utafiti huu umeegemea kwenye mihimili ya nadharia mbili: nadharia ya uhalisia na ya mtindo. Uteuzi wa sampuli ulikuwa wa kimaksudi. Data ya utafiti huu ilikusanywa kwa kusikiliza kanda za nyimbo za wasanii hawa na kuziainisha katika makundi mawili: za kisiasa na zisizo za kisiasa. Mtafiti ameteua sampuli ya kimaksudi ya nyimbo kumi na tano (15) za kisiasa- nyimbo tano (5) kutoka kila msanii kwa lengo la kuchanganua vipengele vya kimtindo katika kila wimbo wa kisiasa. Wawakilishi Kaunti kumi na sita (16) kutoka kaunti hii waliteuliwa kimaksudi na kuhojiwa ili kupata maoni yao kuhusu maudhui katika nyimbo za kisiasa za wasanii Joseph Kamaru, Kamande wa Kioi na John De’Mathew na athari yake kwa hadhira. Mahojiano hayo yaliongozwa na ratiba ya mahojiano. Mtafiti alinasa kauli zao kwa tepurekoda na kuzitumia zikiwa data ya utafiti huu. Maoni yao yalichanganuliwa ili kubainisha athari za nyimbo za kisiasa za wasanii husika kwa wakaazi wa kaunti ya Murang’a. Uchanganuzi wa data umefanywa kwa njia ya kithamano elezi. Matokeo ya utafiti huu yamedhihirisha kwamba wasanii Joseph Kamaru na John De’Mathew hutumia jazanda, methali, taswira, uhuishi na hurafa katika nyimbo zao za kisiasa katika kuwasilisha ujumbe wa kisiasa. Utafiti huu umebainisha kuwa mitindo hiyo hutumiwa na wasanii kuwapigia upatu wanasiasa, kuihamasisha, kuizindua na kuchochea hadhira yao katika kufanya maamuzi ya kisiasa. Matokeo utafiti huu yatakuwa na manufaa kwa wasomi wa Fasihi Simulizi kuhusiana na dhima ya fasihi katika jamii na vile vile kuhusiana na taaluma ya Elimu – Mtindo.